Friday, August 9

KUTOKUKATA TAMAA/KUSUKUMA JAMBO NI SIRI YA MAFANIKIO


Bwana Yesu asifiwe Kanisa.

Hesabu 25:1 – 5

Basi Israeli akakaa Shitimu, kisha watu wakaanza kuzini pamoja na wanawake wa Moabu; 2kwa kuwa waliwaalika hao watu waende sadakani, sadaka walizowachinjia miungu yao; watu wakala chakula, wakaisujudu hiyo miungu yao. 3Ikawa Israeli kujiungamanisha na Baal-peori; hasira za BWANA zikawaka juu ya Israeli. 4Kisha BWANA akamwambia Musa, Watwae wakuu wote wa hao watu, ukamtungikie BWANA watu hao mbele ya jua, ili kwamba hizo hasira kali za BWANA ziwaondokee Israeli.

Mistari yetu ya ufunguzi inaonyesha mafanikio makubwa kwa Mfalme wa Moabu dhidi ya Waisrael.
Maana alifanikiwa kuwachonganisha Waisrael na Mungu wao na WIVU wa Mungu uliwaua Waisrael ishirini na nne elfu.

Unapozungumzia Israel ni taifa teule la Mungu lililotolewa Misri kwa mkono wa Mungu ulio hodari na wenye nguvu.

Kumb 26:8

Bwana akatutoa kutoka Misri kwa mkono wa nguvu, na kwa mkono ulionyoshwa, na kwa utisho mwingi, na kwa ishara, na kwa maajabu;

Hawa ndugu walikwa wana ulinzi wa Mungu wa hali ya juu sana wazungu wanasema (Top security and well protected) lakini walimkosea Mungu kwa KUTOKUKATA TAMAA kwa Mfalme wa Moabu aliyeitwa Balaki.

Ipo mifano mingi sana kwenye Biblia ya watu wema waliofanikiwa kwa kutokukata tamaa na kusukuma maombi yao mpaka wakapata matokeo. Kwenye somo hili natumia mfano wa mtu mbaya kufundishia.

Ukianzia na sura ya 22 ya kitabu cha Hesabu utaona Mfalme Balaki alivyowaogopa wana wa Israel nakutaka Baalamu awalaani ili awafukuze katika nchi yake.

Hesabu 22: 1 – 6 

1 wana wa Israeli wakasafiri na kupanga katika nchi tambarare za Moabu ng'ambo ya pili ya Yordani karibu ya Yeriko.
2 Na Balaki mwana wa Sipori akaona mambo yote ambayo Israeli wamewatendea Waamori.
3 Moabu akawaogopa hao watu sana, kwa kuwa walikuwa wengi; Moabu akafadhaika kwa sababu ya wana wa Israeli.
4 Moabu akawaambia wazee wa Midiani, Sasa jeshi hili la watu litaramba vitu vyote vinavyotuzunguka, kama vile ng'ombe arambavyo majani ya mashamba. Na Balaki, mwana wa Sipori, alikuwa mfalme wa Moabu zamani zile.
5 Basi akatuma wajumbe kwa Balaamu mwana wa Beori, hata Pethori, ulio kando ya Mto, mpaka nchi ya wana wa watu wake, kwenda kumwita, akisema, Tazama, kuna watu waliotoka Misri; tazama, wanaufunika uso wa nchi, tena wanakaa kunikabili mimi.
6 Basi, njoo wewe, nakusihi unilaanie watu hawa; maana wana nguvu kunishinda mimi. Labda nitawaweza, tupate kuwapiga, niwafukuze watoke katika nchi yangu, kwa maana najua ya kuwa yeye umbarikiye hubarikiwa, na yeye umlaaniye hulaaniwa.

Kwa hiyo kutokea hapo Mfalme Balaki alimwajiri Balaamu ambaye alikuwa ni mganga maana mstari wa 7 wa Hesabu tunaambiwa Wazee wa Moabu na Midiani walichukua ujira wa uganga mikononi mwao kwenda kwa Balaamu.

Balaki alituma ujumbe kwa Balaamu mara mbili, yaani ujumbe wa kwanza uliposhindwa kumleta Balaamu kwa Balaki, bado Balaki hakukata tamaa akatuma ujumbe wa pili mkubwa, wenye cheo zaidi na ujira mkubwa zaidi.

Ujumbe wa pili ulifanikiwa kumleta Balaamu kwa Balaki.

Hesabu 22: 7 -12 (Ujumbe wa kwanza)

7 Wazee wa Moabu, na wazee wa Midiani, wakaenda, wakichukua ujira wa uganga mikononi mwao; wakamfikilia Balaamu, wakamwambia maneno ya Balaki.
8 Akawaambia, Kaeni hapa usiku huu, nami nitawaletea jawabu kama Bwana atakavyoniambia; wakuu wa Moabu wakakaa na Balaamu.
9 Mungu akamjia Balaamu, akasema, Ni watu gani hawa ulio nao pamoja nawe?
10 Balaamu akamwambia Mungu, Balaki mwana wa Sipori, mfalme wa Moabu, amewatuma kwangu, akisema,
11 Tazama, kuna watu waliotoka Misri, wanaufunika uso wa nchi; basi njoo unilaanie watu hawa; labda nitaweza kupigana nao, na kuwafukuza.
12 Mungu akamwambia Balaamu, Usiende pamoja nao; wala usiwalaani watu hawa, maana wamebarikiwa.

Hesabu 22: 15 – 21(Ujumbe wa pili)

15 Basi Balaki akatuma wakuu mara ya pili, wengi zaidi, wenye cheo wakubwa kuliko wale wa kwanza.
16 Wakamfikilia Balaamu, wakamwambia, Balaki mwana wa Sipori asema hivi, Nakusihi, neno lo lote lisikuzuie usinijie;
17 maana nitakufanyizia heshima nyingi sana, na neno lo lote utakaloniomba nitalitenda; basi njoo, nakusihi, unilaanie watu hawa.
18 Balaamu akajibu akawaambia watumishi wa Balaki, Kama Balaki angenipa nyumba yake imejaa fedha na dhahabu, siwezi kupita mpaka wa neno la Bwana, Mungu wangu, kulipunguza au kuliongeza.
19 Basi sasa nawasihi, kaeni hapa tena usiku huu, nipate kujua Bwana atakaloniambia zaidi.
20 Mungu akamjia Balaamu usiku, akamwambia, Kwa kuwa watu hawa wamekuja kukuita, enenda pamoja nao; lakini neno lile nitakalokuambia ndilo utakalolitenda, basi.
21 Balaamu akaondoka asubuhi, akatandika punda wake, akaenda pamoja na wakuu wa Moabu.

Tunajifunza hapo kutokukata tamaa na gharama kubwa aliyoiingia Balaki kumpata Balaamu. Yamkini Balaki angekata tamaa kwenye jaribio lake la kwanza maana ni Mungu ndiye aliyemzuia Balaamu asiende kwa Balaki, lakini bado Balaki alituma ujumbe mwingine mkubwa zaidi na wenye cheo zaidi kuliko ule wa kwanza bila kujali kuwa kikwazo alikuwa ni Mungu mwenyewe.

Mara ngapi vikwazo vidogo vidogo tu vimekuzuia usifikie ndoto/hatma yako? Kwa taarifa yako Balaki alizuiwa ndoto yake na Mungu mwenyewe lakini bado hakukata tamaa aliendelea kusukuma maombi yake  

Umewahi kujiuuliza ni mara ngapi umekata tamaa baada ya jaribio la kwanza kushindwa yaweza kuwa ni huduma, biashara, ndoa, malezi, kazi,elimu ulipofanya jambo Fulani kwenye hayo maeneo ukashindwa na kuishia hapo hapo.

Na hayo yote kuna gharama kubwa umetumia kuyafanya lakini haukufanikiwa, sikiliza mwana wa Mungu aliye hai wewe ni bora kuliko Balaki, tuma tena maombi kwa ajili ya hiyo kazi, anza tena hiyo huduma, anzisha biashara tena upya, usichoke kuiombea hiyo ndoa yako, usimkatie tamaa huyo mtoto mtafutie shule nyingine, mpe mtaji mwingine lakini kumbuka safari hii ongeza bidii kwenye maombi, kufunga, kumtolea Mungu pasipo kuchoka hakikisha ujumbe wa sasa wa kupeleka maombi yako kwa Mungu ni mkubwa kuliko ule wa kwanza.

Hebu tuendelee kujifunza kwa Balaki ambavyo hakukata tamaa. Baada ya Balaamu kufika kwa Balaki na kuelezwa haja ya Balaki, Balaamu alimpa Balaki masharti magumu na ya kutumia gharama kubwa sana lakini Balaki hakuchoka aliyatekeleza yote.


Ikawa asubuhi Balaki akamchukua Balaamu, akampandisha hata mahali pa juu pa Baali; na kutoka huko akawaona watu, hata pande zao za mwisho.

Huu mstari wa 41 nataka ujifunze kitu Fulani hapa, najua mara nyingi huwa tunakuwa tumeshayaona mafanikio ya kihuduma, biashara, kazi, ndoa, watoto n.k kama Balaki alivyowaona wana Waisrael toka mahali pa juu.

Sisi mahali petu pa juu ni kwenye maombi na huko huwa tunaona mafanikio yetu, shida ni kwamba tunakata tamaa, tunachoka kusukuma maombi mpaka jambo lizaliwe kwenye ulimwengu wa mwili, yamkini umeona ndoa, huduma, biashara, kazi, watoto na mengine mengi ukiwa mahali pa juu (Maombi) lakini havijawa halisi kwenye ulimwengu wa mwili.

Usichoke kuyasukuma kwa maombi mpaka yatokee, jenga madhabahu hapo nyumbani, kazini, kwenye biashara, kwenye huduma na toa sadaka utaona yale uliyoyaona ukiwa mahali pa juu yakitokea kwenye maisha yako.

Balaki alijenga madhabahu saba, na kutoa sadaka ya ngombe saba na kondoo saba mara tatu. Kwa hiyo alijenga jumla ya madhabahu 21, alitoa ngómbe 21 na kondoo 21.

Hiyo ni gharama kubwa sana Balaki aliingia na mara zote toka anatuma ujumbe Mungu ndiye alikuwa anawatetea wana wa Israel kwa kumzuia Balaamu asiende na hata Balaki alipotoa sadaka zote hizi bado ni Mungu alikuwa anamwambia Balaamu awabariki Waisrael.

Gharama ya ibada ya Balaki haikuwa ndogo, ilikuwa kubwa maana ilijumlisha kupanda vilima na kujenga madhabahu na kutoa sadaka za wanyama, na bado atakuwa aalikuwa akimlipa Baalaamu ujira wa uganga mkubwa tu.

Hesabu 23: 1 – 2 (Madhabahu na sadaka za kwanza)

1 Balaamu akamwambia Balaki, Nijengee hapa madhabahu saba, ukaniandalie hapa ng'ombe waume saba, na kondoo waume saba.
2 Balaki akafanya kama Balaamu alivyonena. Balaki na Balaamu wakatoa sadaka, ng'ombe mume mmoja na kondoo mume mmoja juu ya kila madhabahu.

Hesabu 23:15 – 16 (Madhabahu na sadaka za pili)

15 Akamwambia Balaki, Simama hapa karibu na sadaka yako ya kuteketezwa, nami nitaonana na Bwana kule.
16 Bwana akaonana na Balaamu akatia neno kinywani mwake, akasema, Umrudie Balaki, ukaseme hivi.

Hesabu 23: 28 – 30 (Madhabahu na sadaka za tatu)

28  Basi Balaki akamchukua Balaamu akaenda naye mpaka kilele cha mlima Peori, mahali paelekeapo upande wa nyika iliyo chini yake.
29 Balaamu akamwambia Balaki, Haya, unijengee hapa madhabahu saba, kisha uniandalie ng'ombe waume saba, na kondoo waume saba.
30 Basi Balaki akafanya kama Balaamu alivyosema, akasongeza sadaka ng'ombe mume na kondoo mume juu ya kila madhabahu.

Balaki alijua kabisa kwamba Mungu ndiye alikuwa anmzuia Balaamu asiwalaani Waisrael lakini bado aliendelea kusukuma maombi kupitia ibada ya madhabahu na sadaka. Hivi ulishawahi kujiuliza wewe ni mara ngapi umepeleka maombi yako kwa Mungu tena kwa kuyasindikiza na sadaka kubwa na bado yakakwama lakini badala ya kuendelea kungángánia umekata tamaa na kusimama njia panda na kuanza kulalamika yaani kama ni sadaka huyo mtoto nimemtolea lakini Mungu hajajibu, yaani hii ndoa nimeiombea we acha tu, mh hii biashara nimeshazunguka makanisani na kwa watumishi kibao lakini wapi bado mambo hayaendi ni hasara tu.

Ndugu yangu Balaki hakukata tamaa pamoja na Mungu kuwa mtetezi wa Israel bado jamaa aliendelea kutoa sadaka na kujenga madhabahu. Wewe ni mwana wa Mungu na Mungu anasema amekubariki kwa Baraka zote za rohoni ndani yake Yessu Kristo, Mungu hana mpango wa kuzuia maombi yako kama alivyoyazuia ya Balaki.

Waefeso 1:3-4

3 Atukuzwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, aliyetubariki kwa baraka zote za rohoni, katika ulimwengu wa roho, ndani yake Kristo;
4 kama vile alivyotuchagua katika yeye kabla ya kuwekwa misingi ya ulimwengu, ili tuwe watakatifu, watu wasio na hatia mbele zake katika pendo.

Umechaguliwa ndani ya Kristo hii ni haki yako usikate tamaa, usichoke kusukuma maombi  ili kuchukua hizo baraka ili mradi iwe ni katika mapenzi ya Mungu.

Alichokuwa akiomba Balaki hakikuwa katika mapenzi ya Mungu, mapenzi ya Mungu kwa Waisrael ni kubarikiwa na sio vinginevyo.

Ukisoma Hesabu sura ya 24, 23 na 24 mpango mzima wa Balaki ulishindwa lakini tunapoingia sura ya 25 tunaona Balaki akifanikiwa kuwakosanisha wana wa Israel na Mungu wao kwa chakula, zinaa na ibada ya sanamu.

Bwana Yesu asifiwe kama huyu mwovu aliweza kuliangusha taifa teule kwa kutokukata tamaa kwa nini wewe mwenye haki wa Mungu unashindwa ? 

Balaki alibadilisha gia angani akatumia wanawake wa Moabu kuwashinda adui zake
Hesabu 25:1-2

1  Basi Israeli akakaa Shitimu, kisha watu wakaanza kuzini pamoja na wanawake wa Moabu;
2 kwa kuwa waliwaalika hao watu waende sadakani, sadaka walizowachinjia miungu yao; watu wakala chakula, wakaisujudu hiyo miungu yao.

Msatri wa pili “kwa kuwa waliwaalika’’ hapa anazungumzia wanawake wa Moabu waliawaalika Waisrael.

Tusome andiko hili kwenye Biblia Habari Njema (BHN) utanielewa vizuri.

Hesabu 25:1-2

1Waisraeli walipokuwa huko Shitimu, wanaume walianza kuzini na wanawake wa Moabu. 2Wanawake hao waliwaalika Waisraeli washiriki matambiko waliyotambikia miungu yao, nao Waisraeli wakala chakula na kuiabudu miungu yao.

Mpendwa wangu badilisha gia angani kama Balaki, anza kumtumia Roho Mtakatifu katika maombi yako kwani yeye ni msaidizi wetu. Naona hunielewi, neno linasema Mwanamke ni msaidizi wa mwanaume, maana yake sio kwamba msaidizi hana nguvu/uwezo, la hasha ana nguvu na uwezo mkubwa tena kukushinda, bado hujaelewa kasome habari za Samson utaelewa na pia hii habari ya wanawake wa Moabu walivyoweza kuwaangusha Wana wa Israel.

Sisi tunaye Msaidizi ambaye ni bora kuliko wanawake wa Moabu.

Warumi 8:26
Kadhalika Roho naye hutusaidia udhaifu wetu, kwa maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo, lakini Roho mwenyewe hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa.

Wao wanataja wanawake wa Moabu, wao wanataja mtaji mkubwa wa biashara, wao wanataja uzoefu mkubwa wa kazi lakini sisi tunalitaja jina la Bwana.

Ulishawahi kutaka kuingia kwenye biashara fulani uakona utakavyoambiwa, wewe unakuja na mtaji mdogo hivyo, mtu Fulani alishindwa, unaaza biashara ya genge kwa elimu yako hiyo utaweza wewe kweli, utaweza kweli kulipa kodi za serikali vizuri wewe, na kelele nyingi za aina hiyo.

Lakini nakwambia kamwulize Daudi uzoefu wake ulikuwa kuchunga kondoo, kupigana na samba na dubu na mtaji wake ulikuwa kombeo tu lakini alishimshinda Goliati wake.

Usiogope Goliati wako kwa maana yupo ili uwe Mfalme, bila Goliati hakuna Ufalme. Sukuma maombi yako, pambana kwenye maombi.

Zaburi 20: 7-8

7 Hawa wanataja magari na hawa farasi, Bali sisi tutalitaja jina la Bwana, Mungu wetu.
8 Wao wameinama na kuanguka, Bali sisi tumeinuka na kusimama.

Mpendwa Bwana Yesu asifiwe yamkini umekwama mahali hujui ufanye nini, hamna msaada popote, ninachoweza kukwambia songa mbele kama wale wakoma waliodharaulika walivyosonga mbele wakisema ikiwa ni kufa na tufe, ikiwa ni kuishi na tuishi, na ghafla walipofika kwenye kambi ya Washami waliwakuta Washami wamekimbia wameacha kambi yao na kila kitu.

Hawa wakoma walitajirika ghafla na Waisrael wakapata chakula cha kutosha.

2 Wafalme 7: 3-5, 8

3 Basi walikuwapo watu wanne wenye ukoma, penye lango la mji; wakasemezana, Mbona tunakaa hapa hata tufe?
4 Tukisema, Tutaingia mjini, mjini mna njaa, nasi tutakufa humo; nasi tukikaa hapa, tutakufa vile vile. Haya! Twende tukaliendee jeshi la Washami; wakituhifadhi hai tutaishi; wakituua, tutakufa tu.
5 Basi wakaondoka kabla ya mapambazuko, ili waende mpaka kituo cha Washami; na walipofika mwanzo wa kimo cha Washami, kumbe! Hapana mtu.
8 Basi wale wenye ukoma walipofika mwisho wa kituo, waliingia katika hema moja, wakala, na kunywa, wakachukua fedha, na dhahabu, na mavazi, wakaenda wakavificha; wakarudi, wakaingia katika hema ya pili, vile vile wakachukua vitu, wakaenda, wakavificha.

Hivi hawa walikuwa wanhesabika kuwa ni najisi waliweza kusonga mbele, hawakukata tamaa waliweza kutajirika na kuwezesha wana wa Israel kupata chakula badala ya mavi ya njiwa kwanini wewe uliye ndani ya Kristo ushindwe?

Acha kula mavi ya njiwa kwa gharama kubwa songa mbele ingia kambi ya Washami utajirike na kupata chakula cha kutosha hatimaye wanaokuzunguka nao wafaidi.

Wewe ni zaidi ya mshindi, unayaweza yote katika yeye akutiaye nguvu na aliyeko ndani yako ni mkuu kuliko yeye aliye nje.

Balaki kama nilivyosema hakukata tamaa mpaka mwisho, baada ya mbinu ya kwanza kushindwa alibadili mbinu akatumia mbinu ya mafundisho na mwalimu wake hakuwa mwingine zaidi ya Mganga Balaamu.

Neno linasema watu wangu wanaangamizwa kwa kukosa maarifa. (Kwa faida tu soma mstari wote wa 6 wa Hosea 4, usiishee njiani kama tulivyozoea malizia wote uone hasara ya kukosa maarifa mahali inaishia) Ukijua kosa tunalolifanya kwa kukosa maarifa unaweza kulia maana madhara yake ni mabaya sana.

Hosea 4:6

Watu wangu wanaangamizwa kwa kukosa maarifa; kwa kuwa wewe umeyakataa maarifa, mimi nami nitakukataa wewe, usiwe kuhani kwangu mimi; kwa kuwa umeisahau sheria ya Mungu wako, mimi nami nitawasahau watoto wako
.
Hivi wewe huoni ajabu huyu jamaa aliamua kukaa darasani na kusaka maarifa ya jinsi ya kuwaangamiza Waisrael? Kwa nini usikae darasani kwa Roho Mtakatifu upate maarifa ya kutokuangamizwa? 

Kwa nini unakaa kwenye baraza ya wenye mizaha (Zaburi 1) na kuanza kuwasimulia watu magumu ya noda yako, watoto wako, biashara yao, huduma yako, elimu yako n.k.

Balaki aliamua kukaa chini ya mafundisho ya Balaamu Mganga na akafanikiwa, wewe mwana wa Mungu mwenye baraka zote za rohoni, uliyechaguliwa kabla ya misingi ya dunia, Yesu akakufia, Yesu akakupa Roho Mtakatifu, Yesu akakupa jina lake, damu yake na unazo silaha zote za Mungu pale kwenye Waefeso 6 ni nini kinakushinda usikae chini ya Mwalimu Roho Mtakatifu akakupa maarifa ya kufanikiwa pale unapokwama?

Ufunuo wa Yohana 2:14

14 Lakini ninayo maneno machache juu yako, kwa kuwa unao huko watu washikao mafundisho ya Balaamu, yeye aliyemfundisha Balaki atie ukwazo mbele ya Waisraeli, kwamba wavile vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na kuzini.

Hebu omba hii sala fupi Mungu akupe maarifa (Hebu ifanye kuwa sehemu ya ombi lako kwa kila siku na kwa mtu mwingine ambaye unataka apewe maarifa ya Mungu):

Waefeso 1:17-23

17 Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa utukufu, awape ninyi roho ya hekima na ya ufunuo katika kumjua yeye;
18 macho ya mioyo yenu yatiwe nuru, mjue tumaini la mwito wake jinsi lilivyo; na utajiri wa utukufu wa urithi wake katika watakatifu jinsi ulivyo;
19 na ubora wa ukuu wa uweza wake ndani yetu tuaminio jinsi ulivyo; kwa kadiri ya utendaji wa nguvu za uweza wake;
20  aliotenda katika Kristo alipomfufua katika wafu, akamweka mkono wake wa kuume katika ulimwengu wa roho;
21 juu sana kuliko ufalme wote, na mamlaka, na nguvu, na usultani, na kila jina litajwalo, wala si ulimwenguni humu tu, bali katika ule ujao pia;
22 akavitia vitu vyote chini ya miguu yake, akamweka awe kichwa juu ya vitu vyote kwa ajili ya kanisa; ambalo
23 ndilo mwili wake, ukamilifu wake anayekamilika kwa vyote katika vyote.

Kuna Kiongozi fulani wa nchi fulani aliwahi kusema hili neno mara tatu ELIMU ELIMU ELIMU alichokuwa anasisiza ni umhumu wa ELIMU kwa wananchi wa taifa lake, nami leo nakwambia MAARIFA YA MUNGU, MAARIFA YA MUNGU MAARIFA YA MUNGU.

HITIMISHO:

Mafanikio ya Balaki tunayaona kwenye Hesabu 25:1 – 5. Ila soma sura zote kuanzia Hesabu 22, 23,24 na 25 kwa makini.
Kuanzia sura ya 22 mpaka 24 Balaki hakufanikiwa, tunakuja kuona mafanikio yake kwenye sura ya 25.

Hesabu 25 inaanza kwa kuonyesa tu mafanikio ya kuwakosesha Israel kwa Mungu na hatimaye kuangamizwa kwa watu 24,000 kwa wivu wa Mungu. 

Na siri ya mafanikio yake ni kutokukata tamaa, kusukuma maombi na kuwa mbunifu baada ya mbinu ya kwanza kushindwa.

Yawezekana bado unatumia mbinu za kutegemea kuombewa na watu wengine (Kuombewa sio kubaya ila unatakiwa ukuwe na wewe uombee wengine), au kuomba siku ya Jumapili tu ukienda kanisani na mbinu nyingine ambazo hazijakusaidia ni wakati sasa wa kubadili mbinu.

Unabadili vipi mbinu? Nenda kwa Roho Mtakatifu atakufundisha mbinu mpya.

Balaki alifanikiwa katika maaeneo yafuatayo kuwakosanisha Waisrael na Mungu wao:
  • Zinaa ya kimwili
  • Sadaka walizowachinjia miungu yao
  • Uzinzi wa kiroho (Kuabudu miungu mingine)
Hesabu 25: 1-2

1 Basi Israeli akakaa Shitimu, kisha watu wakaanza kuzini pamoja na wanawake wa Moabu;
2 kwa kuwa waliwaalika hao watu waende sadakani, sadaka walizowachinjia miungu yao; watu wakala chakula, wakaisujudu hiyo miungu yao.

Na mafanikio haya yanatokana na mafundisho ya Balaamu ya utoaji wa sadaka ulio bora, zinaa na kuabudu sanamu.

Ndugu yangu tujitahidi kupata mafundisho sahihi ya maarifa ya Mungu ili tuweze kupata mafanikio katika mambo yote.

3 Yohana 1:2

Mpenzi naomba ufanikiwe katika mambo yote na kuwa na afya yako, kama vile roho yako ifanikiwavyo.

Frank Riessen

0754809462



No comments:

Post a Comment

Barikiwa kwa ujumbe wako.